Hii ni tovuti ya maandishi pekee ambayo inatumia data kidogo. Tazama toleo kuu la tovuti likijumuisha picha na video zote.

Bofya kuelekea tovuti kuu

Pata maelezo zaidi kuhusu toleo hili la linalotumia kiasi kidogo cha data

Lissu: Kauli zangu zilinyofolewa nje ya muktadha

Nia yangu ilikuwa kuwaelewesha watia nia wa chama changu kuhusu matatizo ya mfumo wetu wa uchaguzi.

Muhtasari

Moja kwa moja

Elizabeth Kazibure, Rashid Abdallah & Asha Juma

  1. Lissu: Kauli zangu zilinyofolewa nje ya muktadha

    Nilisema hivi: mabadiliko yanahitaji muda, na kama kweli kulikuwa na utayari wa kufanya mageuzi, basi uchaguzi ungeweza kuahirishwa ili kutoa nafasi ya kuyatekeleza. Hata hivyo, CCM ilikataa kabisa wazo hilo.

    Matokeo yake, watu waliuawa. Kwa mujibu wa Tume ya Jaji Chande, watu 518 walipoteza maisha, huku hatima ya wengine ikiwa haijulikani. Ninaamini kuwa kama uchaguzi ungeahirishwa, maafa hayo yangeweza kuepukika.

    Baadaye nikaelezwa kuwa nilisema "nitakinukisha" na kwamba nilihamasisha maandamano. Lakini maneno hayo yalinyofolewa ‘nje ya muktadha’.

    Katika mazungumzo yale, sikuzungumzia tutaifanyaje serikali hii. Hayo hayakuwa sehemu ya ajenda yangu.

    Leo ninaambiwa nilikuwa na nia ya kuitishia serikali. Ilitoka wapi? Mliambiwa na nani?

    Nia yangu ilikuwa kuwaelewesha watia nia wa chama changu kuhusu matatizo ya mfumo wetu wa uchaguzi ili waweze kuelewa na kuunga mkono msimamo wa CHADEMA wa "No Reforms, No Election".

    Haikuwa kuitishia serikali, kwa sababu hilo halikuwa lengo wala ajenda yangu.

    Sikuhamasisha watu kufanya fujo. Mimi ni mwanasheria, na hakuna sheria yenye masuala ya "kukinukisha."

    Kusudi letu lilikuwa kuwaelimisha na kuwahamasisha Watanzania nchi nzima.

    Tutakapokutana kesho kutwa, nataka niwapitishe kwenye ushahidi uliowasilishwa mbele yenu muone kama unajitosheleza kunyonga mtu.

    Kwa kuwa muda umeisha, naomba niishie hapa kwa leo. Tukutane tena Jumatano.

    Zaidi soma hapa:

  2. Lissu: Mfumo wa uchaguzi unaitetea CCM

    Lissu: Kwa hiyo mfumo wa kampeni wa uchaguzi umekaa katika namna inayoipendelea CCM. Kuna fujo sana. Mimi nimefanyiwa fujo, nimepigwa na mabomu ya polisi Tarime, Serengeti, nimesimamishiwa kampeni kwa siku kumi.

    Mfumo mzima wa kampeni unaumiza upinzani.

    Majaji, nilizungumza na watia nia kuhusu maadili ya uchaguzi. Utafikiri wanapenda maadili ya uchaguzi, lakini ni silaha nyingine ya kuchangia uonevu. Wanaosimamishiwa kampeni ni wapinzani halisi.

    Wale ambao si upinzani wa kweli hawana shida nao.

    Nilizungumza juu ya masuala ya media na election. Majaji, vyombo vya habari vya nchi, vya serikali na visivyo vya serikali, vyote vinakuwa CCM wakati wa uchaguzi.

    Mwaka 2020, ripoti ya utazamaji wa ndani wa uchaguzi ya Research for Independent Democracy Tanzania, iliyoandikwa na Makamu wa Rais wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, iliandika kitu muhimu sana, kwamba vyombo vya habari vyote wakati wa uchaguzi ni CCM.

    BBC walilipishwa faini ya zaidi ya milioni kumi kwa kufanya interview na mimi na TCRA. Jambo TV yenyewe imefungiwa mara nyingi sana na TCRA.

    Masuala yanayohusu siku ya uchaguzi, hilo somo nimelizungumza kwenye mihadhara mingi na matatizo yake. Mnabadilishiwa matokeo, ukishinda kishambashamba wanakubadilishia matokeo, ukipinga unakutana na FFU.

    Hayo ndiyo matatizo ya wagombea wa udiwani na urais niliyoyazungumza nao pale.

    Nilizungumza nao kuhusu what happens baada ya uchaguzi. Kimsingi, nilichowaambia ni kwamba mahakamani haiwezekani kwa sababu hizo taratibu za kutengua matokeo ya uchaguzi, kwa sababu the law is designed in such a way, ina-defend CCM.

    Licha ya kuwa matatizo ya uchaguzi ni makubwa na kila mtu anafahamu.

    Nikawaambia hii ndiyo reform tunayoipigania, hii ndiyo tunayoitaka, na hii ndiyo ya kuwahamasisha Watanzania waidai.

    Soma pia:

  3. Lissu: Mgombea wa upinzani hashindani na wapinzani pekee

    Lissu: Mama amepata asilimia 98 ya kura, lakini swali langu ni: kura hizo zilipatikana kutoka kwa wapiga kura gani, na kwa utaratibu gani?

    Haya ni baadhi ya masuala ambayo yamekuwa yakizungumzwa kwa muda mrefu katika ripoti mbalimbali za waangalizi na wasimamizi wa uchaguzi.

    Pia tulizungumza na watia nia kuhusu mchakato wa uteuzi wa wagombea na namna baadhi yao walivyoenguliwa katika chaguzi tofauti.

    Nilieleza jinsi sheria na mamlaka za uchaguzi zinavyotumika kuwaengua wagombea wa upinzani.

    Katika historia ya uchaguzi nchini, sijawahi kuona wagombea wa CCM wakienguliwa kwa kiwango kinachoonekana kwa wagombea wa upinzani. Hilo ndilo lilikuwa moja ya maeneo ya mjadala wetu kuhusu mfumo wa uchaguzi.

    Nilizungumza pia kuhusu mazingira ya kampeni za uchaguzi.

    Waheshimiwa Majaji, kwa uzoefu wetu wa kushiriki uchaguzi, mgombea wa upinzani hukutana na changamoto nyingi wakati wa kampeni.

    Mara nyingi hulazimika kushughulika na vikwazo vinavyotokana na mamlaka mbalimbali za serikali katika maeneo anayosafiri kufanya kampeni.

    Nilieleza kuwa, kwa mtazamo wangu, mgombea wa upinzani hukabiliana na mfumo mpana unaojumuisha wasimamizi wa uchaguzi, vyombo vya dola na maafisa mbalimbali wa serikali.

    Changamoto hizo, kwa mujibu wa maelezo yangu, zinaweza kuathiri usawa wa ushindani wa kisiasa wakati wa uchaguzi.

    Aidha, nilisema kuwa mgombea wa upinzani anaposhiriki uchaguzi hukutana na ushindani ambao hauhusishi wagombea wengine pekee, bali pia mifumo ya usimamizi wa uchaguzi iliyopo.

    Maelezo zaidi:

  4. Lissu: Shahidi wa mashtaka ndiye aliyechapisha video

    Lissu: George Bagyemu ndiye aliyeniambia makosa niliyokuwa nashtakiwa nayo.

    Kuhusu suala la uchapishaji, kwa mujibu wa ushahidi uliowasilishwa mahakamani, shahidi pekee aliyekuwepo mkutanoni, aliyeyaona na kuyasikia maneno yangu moja kwa moja ni PW17.

    Mashahidi wengine wote hawakuwepo katika mkutano huo.

    PW17 ndiye aliyeieleza mahakama kuwa alirekodi mkutano huo, akaifanyia uhariri na baadaye akaichapisha katika mitandao ya kijamii kupitia video zilizorekodiwa kwa kamera.

    Kuhusu uchapishaji wenyewe, PW17 alisema wazi kuwa yeye ndiye aliyefanya hatua zote za uchapishaji. Kwa maneno mengine, he did everything, si mimi.

    Alipoulizwa nani aliyemualika, alisema aliwasiliana na Mkurugenzi wa Jambo TV, John Maro, ambaye naye alielekezwa na afisa wa CHADEMA, Brenda Rupia.

    Maelezo hayo yote yalikuwa mikononi mwa vyombo vya uchunguzi tangu tarehe 8 Aprili.

    Walikuwa wanajua nani aliandaa mkutano na nani alichapisha maudhui yake. Hata hivyo, wananituhumu kuandaa mkutano ambao uliandaliwa na Naibu Katibu Mkuu wa chama, na pia wananituhumu kuchapisha maneno ambayo, kwa mujibu wa ushahidi wa shahidi wao wenyewe, yalichapishwa na mtu mwingine.

    Mwishowe wakafungua kesi dhidi yangu, na leo nimekaa gerezani kwa zaidi ya mwaka mmoja.

    Sasa, nilizungumza nini katika mkutano huo?

    Majaji, katika saa hizo takribani tatu, nilizungumza na watia nia kuhusu mfumo wa uchaguzi nchini.

    Niliwaeleza changamoto zilizopo katika Katiba ya nchi, sheria za uchaguzi na namna mfumo wa usimamizi wa uchaguzi ulivyojengwa.

    Pia nilizungumzia muundo wa Tume ya Uchaguzi na hoja mbalimbali zinazotolewa kuhusu uhuru wake.

    Kwa mfano, niliwatajia aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi, Jaji Augustino Ramadhani, na mjadala uliowahi kuwepo kuhusu ushiriki wake katika siasa.

    Aidha, nilitoa mfano wa mgawanyo wa majimbo ya uchaguzi kati ya Tanzania Bara na Zanzibar.

    Niliwaeleza kuwa Dar es Salaam ndiyo mkoa wenye idadi kubwa ya wakazi nchini, lakini Zanzibar ina uwakilishi mkubwa wa majimbo ukilinganisha na idadi yake ya watu.

    Hoja yangu ilikuwa kwamba mfumo wa ugawaji wa majimbo haujazingatia idadi ya watu pekee, bali pia vigezo vingine vya kijiografia na kiutawala ambavyo vimekuwepo tangu zamani.

    Soma zaidi:

  5. Lissu: Nilivamiwa na kukamatwa nikiwa nahitimisha mkutano Songea

    Lissu: Tarehe 4 Aprili 2025, mimi na John Heche tulianza ziara ya kusini kwa kuanzia mkoani Lindi. Akiwa huko, Askofu wa Jimbo la Lindi alitupa nafasi ya kukutana naye na tukamueleza msimamo wetu kuhusu ajenda ya "No Reforms, No Election." Baada ya mazungumzo hayo alinipa rozari, ambayo bado ninaivaa hadi leo.

    Baadaye tulielekea mkoani Ruvuma. Tarehe 9 Aprili, majira ya saa kumi na mbili jioni, nilikuwa nikihitimisha mkutano wangu wa hadhara pale Songea, ghafla polisi walivamia mkutano huo.

    Mimi na viongozi wenzangu tulipigwa na kukamatwa, kisha nikapelekwa katika Kituo cha Polisi Songea.

    Baadaye nilipelekwa katika ofisi ya Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Ruvuma (RPC), Michael Chiriwa. Wakati huo nilikuwa na njaa sana, hivyo nikaomba dada yangu aruhusiwe kuniletea chakula. Baada ya kuwasiliana naye, alifika na chakula na nikala nikiwa ofisini kwa RPC.

    RPC Chiriwa aliniambia kwamba ningesafirishwa kwenda Dar es Salaam usiku huo huo kwa maagizo yaliyotoka Makao Makuu ya Jeshi la Polisi.

    Usiku huo nilipakiwa kwenye gari la polisi na kuanza safari ya kuelekea Dar es Salaam. Mmoja wa maafisa aliyekuwa kwenye msafara huo alijitambulisha kwangu kama RCO Makunja.

    Tulisafiri usiku kucha hadi Dar es Salaam, ambapo nilifikishwa mahabusu katika Gereza la Shimoni.

    Soma zaidi:

  6. Lissu: Tulizungumza hadharani, Hatukuwa na mpango wa uhaini

    Lissu: Nilialikwa Chuo Kikuu cha Makerere nchini Uganda mwezi Machi 2025 kutoa mhadhara kuhusu urithi wa Mwalimu Julius Nyerere na nafasi yake katika Afrika Mashariki.

    Katika mhadhara huo nilizungumzia mchango wa Nyerere pamoja na changamoto za mfumo wa uchaguzi ambazo Tanzania inaendelea kukabiliana nazo.

    Baadaye nilialikwa Luanda, Angola. Niliporejea Tanzania baada ya takribani wiki moja, tulipanga kuanza ziara ya kitaifa kueleza msimamo wa "No Reforms, No Election".

    Ziara hiyo ilianza tarehe 22 Machi na kuhitimishwa tarehe 31 Machi 2025, ikihusisha mikutano ya hadhara katika maeneo mbalimbali nchini. Tulizungumza hadharani bila kuficha jambo lolote.

    Hatukuwa na mpango wa kufanya uhaini. Kila tulichokuwa tukifanya kilikuwa wazi kwa umma.

    Nilihitimisha ziara hiyo Iringa tarehe 31 Machi. Nikiwa huko, Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Amani Golugwa, alinifikishia taarifa kwamba chama kilikuwa kimeandaa kikao cha watia nia kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.

    Lengo lilikuwa kujadili namna ya kuwapa maelekezo watia nia hao kuhusu msimamo wa chama wa "No Reforms, No Election".

    Tukakubaliana kuwa tukirejea Dar es Salaam tarehe 3 Aprili, tungezungumza nao na kuwaeleza msimamo rasmi wa chama.

    Mimi na John Heche tulimaliza ziara tarehe 31 Machi na kurejea Dar es Salaam tarehe 1 Aprili.

    Tarehe 3 Aprili 2025 ndipo kikao hicho kilifanyika, ambacho baadaye kikawa sehemu ya msingi wa kesi hii.

    Katika kikao hicho, mimi ndiye nilikuwa mzungumzaji mkuu kwa sababu jukumu la Mwenyekiti wa chama ni kuelezea na kutetea misimamo ya chama.

    Kikao hicho kiliandaliwa na Sekretarieti ya chama chini ya Katibu Mkuu, si Mwenyekiti wa chama.

    Mimi niliarifiwa tu kuwa kutakuwa na kikao hicho kupitia Naibu Katibu Mkuu. Kwa hiyo, madai kwamba Mwenyekiti wa Taifa ndiye aliyeandaa mkutano huo yanaonesha kutoeleweka kwa mfumo wa uendeshaji wa chama.

    Majaji, ushahidi uliotolewa mahakamani na mashahidi 17 unaonesha kuwa mkutano huo ulikuwa mrefu.

    Mimi mwenyewe sikumbuki nilizungumza kwa muda gani. Hata video inayodaiwa kurushwa na Jambo TV sijawahi kuitazama hadi leo.

    Hata mngeniuliza nilizungumza kwa muda gani, nisingeweza kusema kwa uhakika. Ninachoweza kusema ni kwamba nilizungumza kwa muda mrefu sana.

    Katika ushahidi wangu, nitaeleza kwa muhtasari yale niliyoyasema ili mahakama iamue yenyewe kama yalikuwa ya uhaini au la.

    Mimi ni mzungumzaji wa muda mrefu, jambo ambalo naamini wengi wameliona. Watu waliouliza maswali walijibiwa, na ndiyo maana mkutano huo ulidumu kwa muda mrefu.

    Inawezekana ulikuwa wa saa nne au tano, kwa sababu ulikuwa mrefu sana.

    Kama shahidi PW17 alivyosema, ni kweli Jambo TV walikuwepo. Tulikuwa tumefanya kazi nao kwa muda mrefu, na pia kulikuwa na vyombo vingine vya habari.

    Pia unaweza kusoma:

  7. Lissu: CHADEMA ilihamasisha ‘No Reforms, No Election’ Nchi Nzima

    Baada ya hapo, tulianza kuandaa mkakati wa kutekeleza sera ya "No Reforms, No Election". Tulifanya kikao Bagamoyo na kukubaliana kutumia njia zinazotambuliwa kisheria, ikiwemo mikutano ya hadhara, kampeni za uhamasishaji, maandamano ya amani na hatua nyingine za kidemokrasia.

    Tulikubaliana kuwa tungehamasisha wananchi kutumia haki zao za kikatiba kwa njia za amani. Hatukupanga kutumia vurugu wala kuharibu mali za mtu yeyote.

    Aidha, tuliona ni muhimu kuzungumza na makundi mbalimbali ya Watanzania. Tulianza kwa taasisi za kidini na kukutana na viongozi wa Kiislamu kutoka Shura ya Maimamu na taasisi nyingine za Kiislamu.

    Pia tuliomba kukutana na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) pamoja na Baraza la Kikristo Tanzania (CCT), ingawa hatukufanikiwa kufanya mikutano hiyo.

    Tulikutana pia na Jukwaa la Wahariri Tanzania pamoja na viongozi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) ili kuwaeleza msimamo wetu.

    Kwa kuwa Tanzania ina marafiki na washirika katika ukanda huu, tuliamua pia kuonana na baadhi ya viongozi wa kikanda. Mimi, John Heche na Godbless Lema tulisafiri kwenda Nairobi na kukutana na Raila Odinga.

    Vilevile tulikutana na baadhi ya wazee wa taifa, akiwemo Jaji mstaafu Joseph Warioba, na kuzungumza naye kuhusu hoja ya "No Reforms, No Election".

    Kwa ujumla, tulifanya kila tulichoweza kuhakikisha kuwa msimamo wetu unaeleweka kwa umma kwa njia ya wazi na ya amani.

    Pia unaweza kusoma:

  8. Lissu: 'No Reforms, No Election' haikuwa kauli yangu pekee

    Lissu: Mwezi Desemba 2024 ndipo kauli ya "No Reforms, No Election" ilipoibuka rasmi ndani ya CHADEMA.

    Tulijiuliza tufanye nini katika mazingira hayo, na tukakubaliana kwenda kuzungumza na Watanzania kuhusu msimamo wetu ili marafiki na wapinzani wetu wote wauelewe.

    Tarehe 10 Desemba 2024, msimamo huo ulitangazwa rasmi chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa CHADEMA wakati huo, Freeman Mbowe.

    "No Reforms, No Election" si kauli ya Lissu, bali ilikuwa msimamo wa Mwenyekiti wa CHADEMA wakati huo, Freeman Mbowe.

    Katika vikao vya chama tulijadili namna ya kutekeleza msimamo huo. Wakati huo tulikuwa tunakaribia uchaguzi mkuu wa chama uliopangwa kufanyika Januari 2025, hivyo tukakubaliana kuumaliza kwanza kabla ya kuendelea na hatua nyingine.

    Majaji, tarehe 20 Januari 2025 tulifanya kikao cha Baraza Kuu la CHADEMA, ambalo kimsingi ni chombo kikuu cha maamuzi ya chama.

    Kamati Kuu iliwasilisha mapendekezo ya kuifanya sera ya "No Reforms, No Election" kuwa msimamo rasmi wa chama. Baraza Kuu lilikubali mapendekezo hayo na kuyapeleka kwenye Mkutano Mkuu wa chama uliokuwa ufanyike siku iliyofuata, tarehe 21 Januari 2025.

    Tarehe 21 Januari 2025, Mkutano Mkuu ulijadili na kupitisha rasmi sera ya "No Reforms, No Election". Wakati huo Freeman Mbowe alikuwa Mwenyekiti wa chama, nami nilikuwa Makamu Mwenyekiti.

    Katika mkutano huo pia tulifanya uchaguzi wa viongozi wa chama kwa uwazi, huku waangalizi mbalimbali wakialikwa kufuatilia mchakato huo. Baadaye nilichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa CHADEMA.

    Kufuatia uchaguzi huo, nilimteua John Mnyika kuendelea kuwa Katibu Mkuu wa chama pamoja na viongozi wengine katika nafasi mbalimbali.

    Soma zaidi:

  9. Lissu asimulia mchakato wa maridhiano na CCM

    Lissu: Baada ya kushambuliwa kwa risasi wakati wa utawala wa Rais John Magufuli, nilikwenda uhamishoni. Nilinusurika kuuawa na hatimaye nikakimbilia katika Ubalozi wa Ujerumani.

    Tarehe 17 Februari 2022, Rais Samia Suluhu Hassan alipokuwa katika ziara barani Ulaya kwa mkutano uliowakutanisha viongozi wa Umoja wa Ulaya (EU) na Umoja wa Afrika (AU), nilipokea ujumbe kupitia watu wangu kwamba alikuwa anataka kuonana nami.

    Wakati huo, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alikuwa gerezani kwa takribani miezi sita au saba akikabiliwa na kesi ya ugaidi.

    Nilipopata ujumbe huo, nilishauriana na viongozi wenzangu. Tuliona ilikuwa ni hatua nzuri, hivyo nikaenda kukutana naye. Aliniambia alikuwa na nia ya kuyamaliza matatizo yaliyokuwa yamejitokeza wakati wa utawala uliopita.

    Nikamwambia aanze kwa kumwachilia Mwenyekiti wetu, Freeman Mbowe, ndipo mazungumzo mengine yaweze kuendelea. Pia nikasema tunahitaji kuzungumzia Katiba Mpya na Tume Huru ya Uchaguzi. Alijibu kuwa alikuwa tayari kufanya mazungumzo hayo.

    Aidha, nilimweleza kuwa mimi, Godbless Lema na wengine tulikuwa tumekimbia nchi kutokana na hofu ya usalama wetu, hivyo tulihitaji uhakikisho kwamba ilikuwa salama kurejea nyumbani. Baadaye, alitangaza bungeni kuwa Watanzania waliokuwa uhamishoni warejee nchini. Mbowe naye aliachiwa huru, jambo lililotupa faraja ya kurudi nyumbani.

    Tuliporejea, tulipendekeza kuwa watu wote waliokuwa wamefunguliwa kesi ambazo tuliamini zilikuwa na misingi ya kisiasa wafutiwe mashtaka, na baadhi ya kesi hizo zilifutwa.

    Baadaye yakaanza mazungumzo kati ya CHADEMA na CCM. Tulipeleka mapendekezo mbalimbali kuhusu Katiba Mpya, muundo wa Tume Huru ya Uchaguzi na ratiba ya utekelezaji wa mageuzi hayo.

    Kwa upande wetu, tulitaka mchakato wa Katiba Mpya ukamilike kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2025. Hata hivyo, tulianza kuona hakuna hatua za kutosha zilizokuwa zinachukuliwa. Mara nyingi tuliwasilisha mapendekezo kwa maandishi lakini majibu yalitolewa kwa njia ya mazungumzo badala ya maandishi rasmi.

    Takribani mwaka mmoja ulipita bila majibu rasmi ya maandishi kuhusu mapendekezo yetu.

    Mwaka 2025, tuliendelea kusisitiza kuwa majibu yatolewe kwa maandishi ili kuwe na uwazi kuhusu mambo yaliyokubaliwa na yaliyokataliwa.

    Tarehe 21 Mei 2025, tulipokea majibu ya maandishi yaliyokataa mapendekezo yetu yote.

    Baada ya hapo, tulikaa na kujiuliza maana ya maridhiano ikiwa hakuna makubaliano yanayotekelezwa zaidi ya vikao vya mazungumzo. Tukafikia hitimisho kwamba ni lazima kurejea kwa wananchi.

    Tarehe 31 Mei 2025, tuliamua kama chama kuanzisha kampeni ya kuhamasisha madai ya Katiba Mpya na Tume Huru ya Uchaguzi. Tulizunguka nchi nzima kuzungumza na wananchi kuhusu masuala hayo.

    Kadiri joto la kisiasa lilivyoongezeka, ndivyo madai ya kukamatwa kwa wanachama na viongozi wa upinzani pamoja na kesi mbalimbali yalivyoendelea kujitokeza.

    Hali hiyo iliendelea hadi uchaguzi wa serikali za mitaa na vijiji wa Novemba 2024.

    Ndani ya chama kulikuwa na mjadala mkubwa kuhusu kushiriki au kutoshiriki uchaguzi huo kutokana na kutokuwepo kwa mageuzi yaliyokuwa yanadaiwa. Hatimaye, CHADEMA iliamua kushiriki.

    Lissu alidai kuwa uchaguzi huo ulisimamiwa na mfumo wa utawala wa serikali kupitia TAMISEMI, huku watendaji mbalimbali wa uchaguzi wakiwa ni wateule wa mamlaka ya serikali.

    Pia alidai kuwa wagombea wengi wa upinzani walienguliwa katika maeneo mbalimbali ya nchi, hali ambayo, kwa mujibu wake, iliathiri ushindani wa kisiasa katika uchaguzi huo.

    Lissu alidai kuwa wagombea wengi wa upinzani walienguliwa katika maeneo mbalimbali ya nchi, hali ambayo, kwa mujibu wake, iliathiri ushindani wa kisiasa katika uchaguzi huo.

    Alisema waliopinga matokeo hayo walikumbana na nguvu za dola katika maeneo mbalimbali, akidai kuwa watu kadhaa waliuawa Tarime.

    Baada ya uchaguzi huo wa Novemba 28, wiki iliyofuata, tarehe 3 Desemba, Kamati Kuu ya CHADEMA ilikutana kujadili hatua za kuchukua kufuatia yaliyotokea katika uchaguzi na mazingira ya kisiasa yaliyokuwepo nchini.

    Pia unaweza kusoma:

  10. Lissu: Masuala ya uchaguzi si ya kuyachukulia kwa wepesi

    Lissu: Majaji, masuala ya uchaguzi, Katiba na uendeshaji wa nchi yasipowekwa sawa yanaweza kusababisha maafa.

    Leo, mtu anayezungumzia masuala hayo hawezi kuonekana kama chawa. Kabla ya Oktoba mwaka jana, mtu aliyesema hivyo mara nyingi alionekana kwa mtazamo huo.

    Sisi ni Jamhuri ya Muungano, lakini wengi wetu hatufundishwi historia yake kwa kina. Watu wengi hufahamu tu majina ya Mwalimu Julius Nyerere na Sheikh Abeid Amani Karume bila kuelewa mazingira yaliyopelekea kuundwa kwa Muungano.

    Inaitwa Jamhuri ya Muungano kwa sababu Zanzibar ilipitia Mapinduzi ya mwaka 1964, yaliyotanguliwa na migogoro mikubwa ya kisiasa na uchaguzi. Ushahidi wangu ni Ripoti ya Tume ya Jaji Francis Nyalali ya mwaka 1991.

    Tume hiyo ilieleza kuwa, baada ya wananchi wa Zanzibar kuchoshwa na hali ya kisiasa ya wakati huo, kulitokea mapinduzi yaliyoambatana na umwagaji wa damu. Kwa hiyo, historia ya Jamhuri hii inaonesha madhara yanayoweza kutokea pale malalamiko ya kisiasa na uchaguzi yanapopuuzwa.

    Tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992, tumekuwa tukishuhudia malalamiko kuhusu uchaguzi na madai ya kutotendewa haki katika ushindani wa kisiasa.

    Ripoti za Tume ya Nyalali, Tume ya Jaji Othman Chande pamoja na ripoti mbalimbali za waangalizi wa uchaguzi zimeendelea kubainisha changamoto hizo kwa miaka mingi.

    Madai ya Katiba Mpya, usawa wa vyama vya siasa na kuimarishwa kwa demokrasia yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara katika mijadala ya kisiasa nchini.

    Katika ushahidi wangu nitaonesha jinsi tulivyojaribu, mwaka 2025, kuhimiza mabadiliko kwa njia za amani ili kuepusha migogoro, lakini hatukusikilizwa.

    Waheshimiwa Majaji, masuala ya uchaguzi si ya kuyachukulia kwa wepesi. Mfumo wetu wa uchaguzi una changamoto ambazo zimekuwa zikijulikana kwa miaka mingi. Changamoto hizo zimeandikwa katika ripoti za ndani na za kimataifa, na mara nyingi zimeambatana na onyo kwamba zisipotatuliwa zinaweza kuendelea kuleta migogoro.

    Soma Zaidi:

  11. Nimesikia Mbowe yuko kwenye uzinduzi wa bwawa, wakati Mwenyekiti wake yuko Ukonga - Lissu

    Mwaka 2005, Rais Benjamin Mkapa aliondoka madarakani na nafasi yake kuchukuliwa na Jakaya Kikwete. Miaka yake ya kwanza madarakani ilikuwa ya vuguvugu la mageuzi ya kisiasa, Lissu amesema.

    Ameendelea kusema kuwa mwaka 2010, uchaguzi ulifanyika chini ya mfumo huohuo wa uchaguzi, na kulizuka malalamiko makubwa, hususan Zanzibar. Kelele za kudai mabadiliko zikawa nyingi.

    Alipochaguliwa kwa muhula wa pili, Kikwete alisema kulikuwa na haja ya kupata Katiba mpya ili kushughulikia changamoto hizo.

    Mwaka 2014, wakati mchakato wa Katiba Mpya ukiwa kwenye hatua za mwisho chini ya Rasimu ya Jaji Joseph Warioba, CCM ilipinga baadhi ya mapendekezo yake. Baadaye, Kikwete alisema masuala hayo yangejadiliwa baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.

    Mwaka 2015, chini ya mfumo huohuo wa uchaguzi, John Magufuli alichaguliwa kuwa Rais akiwa na Samia Suluhu Hassan kama Makamu wa Rais.

    Majaji, nilisahau kutaja kwamba mwaka 2020 nilirudi kutoka uhamishoni ili kushiriki uchaguzi dhidi ya Magufuli kama mgombea urais wa CHADEMA.

    Kwa mujibu wa sheria ya uchaguzi, baada ya matokeo kutangazwa, Tume ya Uchaguzi huchapisha matokeo ya majimbo katika Gazeti la Serikali. Ukiangalia chaguzi zilizopita kabla ya mwaka 2020, utaratibu huo ulikuwa ukifuatwa.

    Hata hivyo, mwaka 2020 matokeo ya urais hayakuchapishwa. Sina uhakika kuhusu uchaguzi uliofuata kwa sababu nilikuwa gerezani, lakini ninaamini kulikuwa na mambo mengi yasiyo ya kawaida.

    Majaji, ukisoma taarifa za waangalizi wa uchaguzi wa kimataifa pamoja na zile za Umoja wa Afrika, utaona walieleza kuwepo kwa dosari mbalimbali katika uchaguzi huo.

    Ripoti ya Tume ya Uchaguzi ya mwaka 2020 iliwasilishwa kwa Rais Samia Suluhu Hassan mwaka 2021. Kwa mujibu wa Lissu, mijadala kuhusu umuhimu wa mageuzi ya kisiasa na kikatiba iliendelea kujitokeza baada ya uchaguzi huo.

    Baadaye, CHADEMA ilianzisha kampeni ya kudai Katiba Mpya. Katika kipindi hicho, Mwenyekiti wa chama, Freeman Mbowe, alikamatwa na kukabiliwa na kesi ya ugaidi iliyodumu kwa miezi kadhaa kabla ya kuhitimishwa.

    "Jana nimesikia Mbowe yuko kwenye uzinduzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, wakati mimi niko hapa Ukonga," alisema Lissu.

    Soma pia:

  12. CCM imekuwa ikikataa mabadiliko ya katiba na tume huru ya uchaguzi - Lissu

    Lissu: Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 1985 ilifanya wasimamizi wa uchaguzi watoke kwenye mfumo wa serikali za mitaa. Wote ni wateule wa Rais na wanafanya kazi kwa niaba ya Rais. Kwa hiyo, hoja yangu ni kwamba mfumo mzima wa uchaguzi unaonekana kuwa chini ya ushawishi wa CCM.

    Haya yote yapo yameelezwa kwenye pendekezo la katiba ya Warioba ambayo ilifanya utafiti kwenye mfumo mzima wa uchaguzi. Matokeo ya mfumo huu yalianza kujitokeza baada ya uchaguzi mkuu wa 1995.

    Sasa mbali na uchaguzi, kelele za mamabdiliko zilikuwa kubwa sana na nimewambia nimefafanya utafiti wa masuala haya kwa miaka mine.

    Na moja ya mapendekezo ya kuboresha yalikuwa ni kwamba yafanyike mabadiliko ya kikatiba na kuwe na tume huru ili yaliyojitokeza 1995 yasijirudie tena. Kwasbabu haya masuala ya CCM yanaweza kuleta uvunjifu wa amani.

    Serikali ya rais Mkapa na CCM ikakataa. Mwaka 1998

    Mkapa akaunda tume ya kuchunguza ya Jaji Kisanga na ikapendekeza kuwe na mabadiliko, Mkapa akakataa na CCM.

    Mwaka 2002 maafa yakajirudia tena na wengine wakakimbilia Msumbiji na maeneo mengine.

    Mkapa akaunda tume nyingine na kumuweka mtu wake amabaye mwaka 2005 uchaguzi akataka kugombea urais na wakamwambia 'ebo wewe si upo kwenye tume?'

    Soma zaidi:

  13. Mfumo mzima wa uchaguzi umetengenezwa na CCM - Lissu

    Lissu: Tumekuwa tukifanya uchaguzi mkuu tangu mwaka 1957. Uchaguzi wa pili ulifanyika Agosti 1960 na ndio uliozaa Bunge la Uhuru. Tangu miaka ya 1960, Tanzania imekuwa ikifanya uchaguzi kila baada ya miaka mitano bila kukosa.

    Majaji, kabla ya mwaka 1995, kati ya mwaka 1965 na 1995, nchi ilifanya chaguzi chini ya mfumo wa chama kimoja. Kuna vijana wengi hapa ambao huenda hawaelewi maana ya mfumo huo. Kulikuwa na mgombea mmoja na sanduku moja la kura; wananchi walipiga kura kwa mgombea huyo pekee.

    Baada ya marekebisho ya mwaka 1992 yaliyoruhusu mfumo wa vyama vingi, Tanzania iliingia katika enzi mpya ya ushindani wa kisiasa. Wakati huo, Rais Ali Hassan Mwinyi aliunda tume iliyopendekeza kuwepo kwa Katiba mpya na Tume Huru ya Uchaguzi.

    Hata hivyo, Katiba iliyopo sasa ilitungwa katika mazingira ya mfumo wa chama kimoja. Kwa mujibu wa Lissu, mapendekezo yaliyohusu Katiba mpya, Tume Huru ya Uchaguzi na wagombea binafsi yalikataliwa na serikali ya wakati huo pamoja na chama tawala.

    Amesema marehemu Rais Mwinyi aliwahi kuandika katika kumbukumbu zake kwamba walikataa pendekezo la Tume Huru ya Uchaguzi na wagombea binafsi kwa lengo la kuokoa chama, hatua ambayo ilizua mvutano mkubwa kati yake na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.

    Lissu amedai kuwa marekebisho ya Katiba ya mwaka 1992 yaliifanya Tume ya Uchaguzi kuwa karibu zaidi na chama tawala kuliko ilivyokuwa hapo awali. Amesema wajumbe wa tume pamoja na wawakilishi wake waliendelea kuwa wateule wa Rais, ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM.

    Aidha, amesema sheria za uchaguzi zimewaweka wasimamizi wa uchaguzi kutoka ngazi za serikali za mitaa na majimbo kuwa watendaji wanaotokana na mfumo wa uteuzi wa Rais.

    "Kwa hiyo, mfumo mzima wa uchaguzi ni wa CCM," alidai Lissu.

    Soma Zaidi Hapa:

  14. Lissu ahoji muktadha wa kauli zinazounda shtaka la uhaini

    Majaji, kwa mtazamo wangu, kesi hii inahusu uchaguzi. Hati ya mashtaka iliyopo mahakamani inanishtumu kuwa nilikuwa na nia ya kuhamasisha watu kuitishia serikali kwa kuwachochea kuvuruga uchaguzi.

    Maneno ninayodaiwa kuyasema yanahusu uchaguzi. Mashahidi wote 17 wa upande wa mashtaka wametoa ushahidi wao kwa kurejea kauli zangu zinazodaiwa kutolewa kuhusu uchaguzi.

    Nyaraka za ushahidi kuanzia B1 hadi D16 pia zinahusu uchaguzi. Hakuna nyaraka hata moja ambayo haizungumzii suala la uchaguzi.

    Kwa hiyo, Majaji, katika sehemu hii ya ushahidi wangu, naomba nizungumzie uchaguzi.

    Mashahidi PW1, PW2, PW3, na kwa kiwango fulani PW16 na PW17, waliieleza mahakama kwamba kauli ninayodaiwa kuitoa na iliyochapishwa kupitia Jambo TV kwenye YouTube ilikuwa sehemu ya video yenye urefu wa takribani saa tatu.

    PW16 na PW17 walisema video hiyo ilikuwa na urefu wa takribani saa mbili na zaidi. Hata hivyo, kwa ujumla wao wote walikubaliana kwamba video hiyo ilikuwa ndefu.

    Kauli zinazodaiwa kuunda msingi wa shtaka la uhaini hazifikii hata dakika moja. Swali langu ni kuwa, katika muda wote uliobaki wa takribani saa tatu, nilizungumza nini?

    Katika sehemu hii ya ushahidi wangu, nataka kueleza mantiki na muktadha wa kauli nilizozungumza katika kipindi hicho mwaka jana.

    Pia unaweza kusoma:

  15. Shahidi asitutoe nje ya reli - Serikali

    Upande wa Serikali: "Sasa ushahidi unaotolewa unatoka nje ya mawanda ya kesi, kwa sababu shahidi analeta masuala yasiyohusiana moja kwa moja na shauri hili. Hii si sehemu sahihi ya kuyajadili.

    Haya masuala ya watu kufa anaweza kuyazungumzia, lakini yanahusiana vipi na kesi iliyopo mbele ya mahakama? Kwa hiyo, naomba majaji, kama inawezekana, wamuelekeze shahidi asitutoe nje ya reli. Hivyo ndivyo sheria inavyotaka."

    Lissu: "Majaji, msingi wa utetezi wangu ni kwamba baadhi ya kesi hizi zimetengenezwa, na hiyo ni sehemu ya tabia ya polisi na waendesha mashtaka.

    Kesi yangu ni uthibitisho kwamba mamlaka yanaweza kutumika vibaya. Sizungumzi mambo haya ili mahakama inionee huruma, bali kuonyesha kwamba kuna tatizo ambalo linahusiana na ushahidi wangu.

    Kusema kwamba tunaweza kutumia wiki mbili kunanitia wasiwasi, kwa sababu wao wamekuwa na mwaka mmoja na miezi kadhaa kuwasilisha upande wao. Leo ninapotaka kutumia muda kujitetea, wanaeleza kuwa napoteza muda. Sipotezi muda, najitetea. Wana wasiwasi gani?"

    Soma Zaidi:

  16. Hii ni mara yangu ya nne kukamatwa chini ya Samia, Lissu amesema

    Kuhusu kesi hii, nilikamatwa tarehe 9 Aprili 2025 na kufikishwa mahakamani siku iliyofuata. Hii ni mara yangu ya nne kukamatwa chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan na polisi wake.

    Safari hii nimefunguliwa kesi ya uhaini. Kufikia sasa, tayari nimekaa gerezani kwa miezi 16 na ninaelekea kutimiza mwezi wa 17, sawa na zaidi ya mwaka mmoja na miezi minne.

    Majaji, hiki ni kipindi kirefu zaidi kuwahi kukaa gerezani katika maisha yangu. Pia ni kipindi kirefu zaidi kwa kiongozi wa CHADEMA kushikiliwa gerezani.

    Aidha, hii ndiyo kesi kubwa zaidi kuwahi kufunguliwa dhidi ya kiongozi wa upinzani tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi nchini takriban miaka 35 iliyopita. Hakuna kiongozi mwingine aliyewahi kufunguliwa kesi ya aina hii.

    Haya yote yamenitokea mimi binafsi. Ninaamini hakuna kiongozi mwingine wa ngazi ya juu wa CHADEMA aliyepitia mateso na changamoto nyingi kama nilizopitia.

    Nina bahati kwamba, licha ya kujeruhiwa na kubaki na ulemavu wa kutembea kwa kuchechemea, bado niko hai. Wapo wengi tuliowahi kufanya kazi pamoja katika kipindi cha miaka kumi iliyopita ambao wengine wameuawa na wengine hadi leo hawajulikani walipo.

    Kama chama, tumepitia nyakati ngumu sana. Tumebeba maumivu makubwa na tumekumbwa na mateso mengi. Mimi binafsi nimefunguliwa kesi mbalimbali ambazo naamini ni za uongo, zikihusisha polisi na mawakili wa serikali.

    Kesi hii si ya polisi pekee, bali inahusisha pia waendesha mashtaka wa serikali. Katika miaka miwili au mitatu iliyopita, tumezika viongozi wengi wa chama.

    Tumepitia maumivu makubwa sana, na mimi binafsi nimeumizwa sana.

    Soma Zaidi Hapa:

  17. Lissu: Mwaka 2024 ulikuwa mgumu kwa viongozi wa CHADEMA

    Mwezi uliofuata September 7 mkesha wake Mkurugenzi wa Hamasa CHADEMA makao makuu, Ally Kibao akatekwa kwenye busi akiwa anakwenda Tanga, akiwa Tegeta alishushwa kwa nguvu.

    Ukiangalia unaona kabisa ni police kulingana na magari yao, ni polisi ambao ni usalama wa taifa. Kesho yake mzee Kibao akaokotwa akiwa ameuawa maeneo ya ufukweni Ununio, inaelekea aliteswa vibaya sana.

    Majaji wakati marehemu Kibao anatekwa nyara na kuuawa kulikuwa na matukio mengi ya viongozi wa CHADEMA kutekwa na kuawa kilikuwa kipindi kigumu sana 2024.

    Katika kupinga hayo yote chama kilisema kitaandamana tarehe 23 September. Ilipotika asubuhi nikavamiwa na jeshi la polisi mapema asubuhi nyumabani kwangu nikakamatwa. Nikawekwa kituo cha polisi Mbweni.

    Nikakaa Mbweni mpaka usiku, kisha wakanirudisha nyumbani kwangu hawakunifungulia mashtaka.

    Majaji, nakumbuka nilisema nilikamatwa Karatu ili nisiende kuonana na wananchi wa Ngorongoro hiyo ilikuwa Machi 2023. Nilienda kuwekwa kituo cha polisi cha Wilaya ya Monduli waheshimiwa majaji, ili tu kuniharibia mipango yangu

    Soma Zaidi Hapa:

  18. Lissu: Siku niliyopigwa risasi walinzi hawakuwepo

    Siku niliyoshambuliwa, walinzi wote hawakuwepo na mageti yalikuwa wazi. Nikiwa kwenye eneo la maegesho ya magari, nilipigwa risasi 16, hali iliyosababisha kufanyiwa operesheni 26. Hadi leo, bado nina risasi moja mwilini, karibu na uti wa mgongo.

    Hakuna mtu aliyekamatwa wala kutuhumiwa kuhusika na tukio hilo. Aidha, sijawahi kuitwa na polisi kueleza kilichotokea siku hiyo. Sidhani hata kama polisi walifungua jalada la uchunguzi (RB).

    Majaji, sikufa. Mungu si Athumani. Sikufa. Badala yake, Magufuli alifariki dunia. Baada ya kifo chake, kesi sita zilizokuwa zimefunguliwa dhidi yangu katika Mahakama ya Kisutu zilifutwa mwezi Septemba 2021.

    Baadaye, Rais Samia Suluhu Hassan aliingia madarakani na kuja na agenda ya 4R.

    Katika kutekeleza agenda hiyo, tarehe 12 Agosti 2024 niliitwa, kwa nafasi yangu ya Makamu Mwenyekiti wa CHADEMA, kushiriki pamoja na Baraza la Vijana la CHADEMA (BAVICHA) katika maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani.

    Jeshi la Polisi lilipiga marufuku maadhimisho ya CHADEMA, lakini ya CCM yaliendelea kufanyika. Nikasema Jeshi la Polisi halina mamlaka ya kuzuia shughuli hizo na kwamba jukumu lake ni kulinda raia.

    Tarehe 12 Agosti 2024 nilisafiri kwa ndege kwenda Mbeya. Nilipowasili, ilikuwa tayari jioni, ndipo nikaelekea katika ofisi za chama ngazi ya kanda.

    Majaji, siku hiyo nilivamiwa na polisi wakiongozwa na Mkuu wa Operesheni, Awadh Juma. Mimi na viongozi wenzangu tulipigwa na baadaye kukamatwa. Baadaye nilipelekwa mkoani Songwe na kuwekwa mahabusu huko.

    Siku iliyofuata mchana, nilisafirishwa kwa gari kurudishwa Dar es Salaam.

    Nilipofikishwa Dar es Salaam, nilikabidhiwa kwa polisi wa Kituo Kikuu cha Polisi (Central) na askari kutoka Songwe na Mbeya. Nilipowauliza kosa langu ni lipi, waliniambia walikuwa wakinipeleka nyumbani. Sikufunguliwa mashtaka yoyote. Hiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kukamatwa chini ya utawala wa Rais Samia.

    Soma Zaidi:

  19. Nilipimwa mkojo kwa mashtaka ya uchochezi - Lissu

    Tarehe 29 Julai, nilikamatwa kwa kosa la kumuita Rais Magufuli "dikteta uchwara", siku tatu baada ya kuachiliwa. Nikasafirishwa usiku na kulazwa Kituo cha Polisi Chamwino, ambako kulikuwa na mbu wengi. Baadaye nikaletwa Dar es Salaam na kushtakiwa kwa uchochezi.

    Septemba mwaka huo, nilikamatwa tena na kuletwa Dar es Salaam. Kufikia mwisho wa mwaka 2016, nilikuwa nimekamatwa mara nne na polisi wa Magufuli, huku kesi zote zikisikilizwa katika Mahakama ya Kisutu.

    Kesi ya nne ilifunguliwa mwezi Desemba mwaka huo huo.

    Majaji, mwaka 2017 nilikamatwa tena Dodoma mwezi Februari. Mwezi Aprili kulikuwa na uchaguzi wa Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS).

    Wanachama walinitaka nigombee. Siku tatu au nne kabla ya uchaguzi, nilikamatwa na kupelekwa Segerea, ambako nilikaa kwa siku nne.

    Siku ya Ijumaa nikapelekwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu. Hakimu alisema kesi hiyo ilikuwa na dhamana na akaniruhusu kwenda kugombea urais wa TLS.

    Baada ya uchaguzi wa TLS, nilikamatwa tena mara mbili, mwezi Juni na Agosti. Katika moja ya matukio hayo, nilipelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali kupimwa mkojo kwa tuhuma za uchochezi, ingawa hadi leo sijui jambo hilo lilihusiana na nini.

    Soma Zaidi:

  20. Lissu: Polisi walitaka kuvunja chumba cha maiti na kuchukua miili

    Mwaka 2005, Jakaya Kikwete aliingia madarakani.

    Mwezi Julai 2011, polisi walifanya mauaji katika Mgodi wa North Mara, Nyamongo. Wananchi wa Nyamongo walinipigia simu wakiniomba niende kuwasaidia kwa sababu polisi walikuwa wanawalazimisha kuzika miili ya waliouawa. Nikasafiri kwenda huko na kudai uchunguzi ufanyike kuhusu mauaji hayo.

    Nilipofika Tarime, nilipata taarifa kuwa polisi walitaka kuvunja milango ya chumba cha kuhifadhia maiti ili wachukue miili. Tulikesha nje ya chumba hicho, na ndipo nilipopigwa sana na kujeruhiwa vibaya.

    Baada ya hapo, nilipewa kesi yangu ya pili ya jinai, ambayo nayo ushahidi wake ulikuwa wa mashaka.

    Mwaka uliofuata, 2012, polisi waliua wananchi kadhaa wakati wa maandamano mjini Arusha. Sheria za nchi hii zinaruhusu maandamano, lakini watu waliuawa. Tukaenda kusisitiza haki itendeke, ndipo mimi na wabunge wenzangu, akiwemo Dk. Slaa, tukakamatwa.

    Baadaye, Rais John Pombe Magufuli aliingia madarakani, na kisha Samia Suluhu Hassan.

    Mwaka 2015, wakati wa uchaguzi mkuu Zanzibar, Seif Sharif Hamad alitangazwa kuwa ameshinda, lakini matokeo yakafutwa.

    Ilipotangazwa kuwa uchaguzi wa marudio ungefanyika mwaka 2016, waandishi wa habari waliniuliza maoni yangu. Nikasema kuwa walikuwa wanataka kuleta maafa. Tarehe 26 Juni 2016, nilikamatwa kwa mashtaka ya uchochezi na kupelekwa mahakamani, lakini mashahidi hawakuletwa tena.

    Hata baada ya kupigwa risasi, mashahidi hawakuwahi kuletwa mahakamani.

    Soma Zaidi Hapa: