Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Tundu Lissu, anaendelea leo, Jumanne Agosti 11, 2026, kumuhoji shahidi wa 16 wa upande wa mashtaka katika kesi ya uhaini inayomkabili katika Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam.
Kesi hiyo, yenye Jalada la Jinai Na. 1 la mwaka 2025, ilianza kusikilizwa Mahakama Kuu baada ya Lissu kushtakiwa kwa shtaka la uhaini linalohusishwa na kauli zake kuhusu kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.
Lissu alikamatwa Aprili 9, 2025, akiwa Mbinga mkoani Ruvuma, na siku iliyofuata akafikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, na kusomewa shtaka la uhaini pamoja na makosa mengine yaliyohusishwa na kauli zake.
Kesi hiyo ilisimama kwa takribani miezi mitano tangu Februari 24, 2026, kabla ya kuanza tena jana, Agosti 10, chini ya Jopo la Majaji watatu likiongozwa na Jaji Dunstan Ndunguru.
Usikilizwaji wa kesi hiyo unaendelea kwa mfululizo kuanzia Agosti 10 hadi Septemba 7, 2026.
Jana, shahidi wa 16, Kamishna Msaidizi wa Polisi Amini Mahamba, alimaliza kutoa ushahidi wake wa msingi. Alieleza mahakama kuhusu upelelezi uliofanywa na polisi, ikiwemo namna walivyopitia video ya hotuba ya Lissu iliyochapishwa na Jambo TV na kauli walizodai zilihusisha kuzuia uchaguzi na kuhamasisha uasi.
Mahamba pia alieleza kuhusu majalada ya uchunguzi kutoka mikoa mbalimbali, kukamatwa kwa Lissu na madai ya vitisho dhidi ya baadhi ya mashahidi wa upande wa mashtaka.
Leo, Lissu ameanza hatua ya cross-examination, ambapo anamuuliza shahidi kuhusu uadilifu wake kama afisa wa polisi, uzoefu wake wa upelelezi na tofauti kati ya ushahidi alioutoa jana na maelezo yake ya awali.
Endelea nasi hapa kwa taarifa za moja kwa moja kutoka Mahakama Kuu Dar es Salaam.