Hatua zetu za kujilinda zinaweza kugeuka kuwa mashambulizi - Iran
Naibu Mkuu wa Masuala ya Kisiasa wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran, Yadollah Javani, amesema hatua zinazochukuliwa na Iran katika vita vinavyoendelea kwa sasa ni za kujilinda, lakini zinaweza kubadilika na kuwa mashambulizi siku zijazo.
Akizungumza katika mahojiano na televisheni na redio ya taifa ya Iran, Javani amesema maadui wa Iran ndio walioanzisha vita hivyo, na kwamba hatua za Iran ni sehemu ya kujilinda.
Iran pia imesema itachukua hatua zote muhimu kulinda nchi na kuzuia vitisho vya maadui, huku ikisema inaweza kubadilisha namna inavyojibu endapo hali itahitaji.
Javani amesema majeshi ya Iran yatachukua hatua mpya kwa kuzingatia maelekezo yatakayotolewa, na kwamba yatachukua hatua zote muhimu kulinda nchi, kuhakikisha usalama na kuzuia vitisho kutoka kwa maadui kwa wakati unaofaa.
Kauli ya Javani imekuja baada ya mshauri wa Kamanda Mkuu wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu, Mohammad Reza Naqdi, kusema Iran imeamua kubadili mkakati wake wa kijeshi kutoka unaolenga zaidi kujilinda hadi unaoruhusu pia kushambulia pale itakapoonekana kuwa ni lazima.
Soma zaidi: