Tume yaanza kuwasaka wapangaji wa ghasia za Uchaguzi Tanzania
Tume iliyoundwa na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kuchunguza wahusika wa ghasia na ukiukwaji wa sheria wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025, imeanza rasmi kazi yake.
Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Mstaafu wa Mahakama ya Rufani, Shaban Ally Lila, amesema Tume inalenga kubaini wahusika wa ghasia hizo, namna walivyohusika pamoja na waliohusika kusababisha vifo, majeraha na watu kupotea wakati na baada ya uchaguzi.
Uchaguzi Mkuu wa Tanzania ulifanyika tarehe 29 Oktoba 2025, lakini katika baadhi ya maeneo kuliripotiwa ghasia na matumizi ya nguvu yaliyosababisha vifo, majeraha na uharibifu wa mali.
Tume hiyo mpya imeundwa kufuatia mapendekezo ya Tume ya awali iliyokuwa ikiongozwa na Jaji Mstaafu Mohamed Chande, ambayo ilichunguza matukio ya ghasia na uvunjifu wa amani yaliyotokea wakati na baada ya uchaguzi.
Kuchunguza matumizi ya silaha
Kwa mujibu wa Jaji Lila, Tume itachunguza madai ya watu kupata majeraha makubwa kutokana na matumizi ya silaha za moto kinyume na sheria, taratibu na miongozo iliyopo.
Pia itachunguza madai ya watu kupigwa risasi nje ya maeneo ya ghasia, pamoja na taarifa za watu waliopotea wakati na baada ya uchaguzi.
Tume pia imepewa jukumu la kuchunguza iwapo nguvu iliyotumika kudhibiti ghasia ilikuwa imezidi kiwango kinachoruhusiwa kisheria.
Miongoni mwa masuala mengine yatakayochunguzwa ni vifo visivyo vya kawaida vya watoto na watu wa makundi maalum vilivyotokana na hatua za kudhibiti ghasia.
Wahusika wa ghasia
Tume inatarajiwa kuchunguza ushiriki wa waliopanga, waliofadhili, walioratibu au kutekeleza ghasia hizo.
Kwa mujibu wa hadidu rejea zake, Tume pia inaweza kuchunguza jambo jingine lolote itakaloona ni muhimu na linaloendana na majukumu yake.
Uchunguzi utafanywa kwa kutumia ushahidi wa moja kwa moja, nyaraka pamoja na taarifa zitakazopatikana wakati wa kutembelea maeneo yaliyokumbwa na matukio hayo.
Tume imesema itazingatia pia haki ya kusikilizwa kwa wale wote ambao wanaweza kuguswa na taarifa zitakazowasilishwa wakati wa uchunguzi.
Tume ina siku 150
Tume hiyo ina makamishna sita na inaongozwa na Jaji Mstaafu Shaban Ally Lila. Makamishna wengine ni Jaji Petrus Tileinge Damaseb wa Namibia, Jaji Barishaki Bonny Cheborion wa Uganda, pamoja na Majaji Wastaafu wa Mahakama Kuu ya Tanzania Gad John Mjemmas, Awadh Mohamed Bawazir na Aishiel Nelson Sumari.
Katibu wa Tume ni Paul Kadushi.
Tume imepewa siku 150 tangu kuzinduliwa kwake kukamilisha uchunguzi na kuwasilisha taarifa yake.
Mwenyekiti wa Tume ametoa wito kwa wananchi, waandishi wa habari na mtu yeyote mwenye taarifa zinazohusiana na hadidu rejea za Tume kuwasilisha taarifa hizo ili kusaidia uchunguzi.
Soma pia: