Israel yatangaza zabuni ya mradi 'tata' wa makazi katika Ukingo wa Magharibi
Israel imetangaza zabuni ya kujenga takriban nyumba 1,200 kwa ajili ya walowezi katika eneo lenye umuhimu wa kimkakati katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu, huku ikijaribu kuondoa kabisa uwezekano wa kuwepo kwa taifa la Palestina.
Mipango ya ujenzi katika eneo linalojulikana kama "E1" huko Jerusalem Mashariki imekuwa ikikosolewa vikali na jumuiya ya kimataifa kwa muda mrefu, na makazi hayo yanachukuliwa kuwa haramu kwa mujibu wa sheria za kimataifa.
Kupitia mpango huu, Ukingo wa Magharibi utagawanywa katika sehemu mbili, na Jerusalem Mashariki itatenganishwa na maeneo mengine.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza, Ed Miliband, alikemea kutangazwa kwa zabuni hiyo akiitaja kuwa "kitendo kisichokubalika na kilicho na madhara" na kuitaka Israel "kusitisha mara moja mipango ya E1, kuondoa zabuni hiyo na kukomesha upanuzi wa makazi ya walowezi."
Tangu Israel ilipokalia kwa mabavu Ukingo wa Magharibi na Jerusalem Mashariki wakati wa Vita vya Mashariki ya Kati vya mwaka 1967, imejenga takriban makazi 160, ambayo ni makazi ya Wayahudi wapatao 700,000.
Wapalestina wanataka maeneo haya, pamoja na Ukanda wa Gaza, kwa ajili ya taifa lao la baadaye.
Hivi sasa, takriban Wapalestina milioni 3.3 wanaishi sambamba na walowezi hao.
Licha ya upinzani mkali kutoka kwa jumuiya ya kimataifa, serikali mfululizo za Israel zimeendelea kuruhusu upanuzi wa makazi hayo.
Maelezo zaidi: