Wanigeria 83 warejea nyumbani kwa kuhofia ghasia dhidi ya wahamiaji Afrika Kusini

Chanzo cha picha, EMMANUEL CROSET / AFP via Getty Images
Kundi la raia 83 wa Nigeria limewasili mjini Lagos usiku wa Jumatano, huku kukiwa na wasiwasi unaoongezeka vurugu dhidi ya wahamiaji nchini Afrika Kusini.
Watu hao walirejea nyumbani wakiandamana na maafisa wawili wa Ubalozi wa Nigeria jijini Johannesburg.
Wizara ya Mambo ya Nje ya Nigeria imrsema kuwa watu binafsi waligharamia usafiri wao, ikiongeza kuwa "zoezi la kurejesha nyumbani kundi hili la watu liliweezeshwa na wahisani wenye nia njema, ambao msaada wao uliwawezesha kuwarejesha salama nchini Nigeria."
Mpango wa serikali wa kurejesha watu kwa hiari ulimalizika rasmi mwezi Julai.
Waigeria 1,500 walirejeshwa nyumbani chini ya mpango huo.
Serikali ilisema safari hizo ziligharamiwa kwa fedha za umma na kwamba watu hao hawakulazimika kulipia safari zao.
Wanigeria wengine 66 walirejea mwezi Juni kwa safari tofauti ya ndege iliyoandaliwa na kugharamiwa na watu binafsi, kulingana na Wizara ya Mambo ya Nje.
Waliowasili hivi karibuni walipokelewa na Balozi Haruna Ali-Gombe, Mkurugenzi wa Idara ya Masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Nigeria.
Kisha walikabidhiwa kwa taasisi husika za serikali kwa ajili ya taratibu za nyaraka na utambuzi kabla ya kuunganishwa tena na familia zao.
Kurejea kwao kunakuja wakati Afrika Kusini inakabiliwa na maandamano mapya dhidi ya wahamiaji wasio na vibali halali.
Baadhi ya makundi yametoa wito kwa wageni wasio na hadhi ya kisheria kuondoka nchini humo na yametoa makataa ya hadi Septemba 30 kwa wahamiaji wasio na vibali kuondoka.
Afrika Kusini imeshuhudia maandamano kadhaa kuhusu uhamiaji mwaka huu, huku waandamanaji wakitaka kuwepo kwa udhibiti mkali zaidi.
Serikali imelaani mashambulizi dhidi ya wahamiaji na kusema inaongeza juhudi za kutekeleza sheria za uhamiaji na kushughulikia uhamiaji usiofuata taratibu.
Mamlaka za Afrika Kusini zinasema zaidi ya wahamiaji 80,000 wasio na vibali wamefurushwa nchini humo kama sehemu ya kampeni pana ya utekelezaji wa sheria.
Serikali inasema itaendelea kuimarisha usalama wa mipakani na kutekeleza sheria za uhamiaji.
Maelzo zaidi:





























