Iran na Marekani kuingia awamu mpya ya vita?

Iran and U.S. flags

Chanzo cha picha, Getty Images

    • Author, شیدا هوشمندی
    • Nafasi, بی‌بی‌سی
    • Akiripoti kutoka, واشنگتن
  • Iliyochapishwa
  • Muda wa kusoma: Dakika 7

Jumatatu, Agosti 17, 2026, iliashiria mwisho wa kipindi cha siku 60 ambacho Iran na Marekani zilipaswa kufikia makubaliano mapana zaidi ya kumaliza vita, kushughulikia mpango wa nyuklia wa Iran na kufungua tena Mlango bahari wa Hormuz. Hata hivyo, si tu kwamba hakuna makubaliano yaliyofikiwa, bali pande hizo mbili sasa zinajiandaa zaidi kuliko wakati mwingine wowote kwa makabiliano ya muda mrefu.

Kadri muda wa siku 60 wa kufikia makubaliano unavyokaribia, vyombo vya habari vya Marekani vimeeleza mikakati miwili inayoonekana kutofautiana kutoka Iran na Marekani katika hatua hii ya vita.

Wakati utawala wa Donald Trump ukizidi kutegemea shinikizo la kiuchumi na kizuizi cha majini ili kuilazimisha Iran kulegeza msimamo, gazeti la Wall Street Journal linasema baadhi ya watu ndani ya mfumo wa uongozi wa Tehran wanaona vipindi vya kusitishwa kwa mashambulizi ya Marekani si kama ishara ya amani, bali fursa ya kujiandaa kwa makabiliano makubwa zaidi.

Wakati huo huo, vyombo vya habari vya Marekani viliibua swali katika ripoti na mijadala yao siku ya Jumapili: Ikiwa vita hivi vimegeuka kuwa mashindano ya muda mrefu ya uvumilivu, Marekani itaweza kubeba kwa muda gani gharama zake za kijeshi, kiuchumi na kiusalama?

Wall Street Journal: Kusitishwa kwa mapigano kulikuwa fursa kwa Iran kujiandaa kwa vita kubwa zaidi

Wall Street Journal, katika ripoti yenye kichwa "Mpango wa Siri wa Iran wa Kuendeleza Vita," iliandika kuwa mawasiliano yaliyodakwa na taarifa nyingine zilizokusanywa na taasisi za usalama katika nchi za Kiarabu zinaashiria mabadiliko katika mkakati wa viongozi wa Iran na maandalizi ya kupanua wigo wa vita.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, baada ya kusainiwa kwa hati ya makubaliano ya maelewano kati ya Iran na Marekani Juni 17, maafisa wa utawala wa Trump walitarajia makubaliano hayo yangefungua njia ya kufunguliwa tena kwa Mlango bahari wa Hormuz na hatimaye kupunguza mvutano.

Hata hivyo, Wall Street Journal, ikinukuu maafisa wa Iran na nchi za Kiarabu, iliandika kuwa baadhi ya viongozi wa Iran walikuwa na mtazamo tofauti kabisa.

Kwa mujibu wa gazeti hilo, kulikuwa na hofu kwamba makubaliano hayo yangeweza kuwa njia pekee ya kupunguza shinikizo kwa uchumi wa dunia na kuwapa Marekani na Israel muda wa kuandaa mashambulizi makubwa zaidi dhidi ya Iran siku zijazo. Kwa sababu hiyo, makundi ndani ya serikali, badala ya kutegemea mazungumzo, yametumia miezi miwili iliyopita kujiandaa kwa vita pana zaidi.

Hauhitaji Whatsapp
BBC Swahili sasa kwenye WhatsApp

Pata habari za kina kutoka BBC News Swahili, moja kwa moja kupitia WhatsApp.

Bonyeza hapa kujiunga

Mwisho wa Whatsapp

Wall Street Journal inaandika kuwa hatua hizo zimejumuisha kuongeza ushawishi wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu (IRGC), kuongeza uzalishaji wa makombora na ndege zisizo na rubani, kupanua shughuli za kijasusi na kupambana na ujasusi, pamoja na kuwateua makamanda wenye historia ya Vita vya Iran na Iraq na ukandamizaji wa ndani kushika nyadhifa muhimu za kiusalama.

Gazeti hilo, likinukuu maafisa wa kijasusi wa nchi za Kiarabu, linaripoti kuwa mawasiliano kati ya Iran na makundi yake washirika nchini Iraq na Yemen yanaonyesha kuwa Tehran sasa inalenga zaidi kuandaa vikosi kwa ajili ya kupanua wigo wa vita na kuongeza gharama kwa Marekani na washirika wake wa kikanda.

Mohammad Hassan Sangtarash, mchambuzi wa masuala ya ulinzi anayeishi Tehran ambaye Wall Street Journal inamtaja kuwa karibu na serikali ya Iran, aliliambia gazeti hilo kuwa kuna mtazamo ulioenea nchini Iran kwamba "vita halisi bado havijaanza."

Alisema baadhi ya viongozi wa serikali ya Iran wanaona yaliyotokea hadi sasa kama ongezeko la mvutano hatua kwa hatua, linalolenga kudhoofisha uwezo wa Iran kabla ya makabiliano makubwa zaidi.

Wall Street Journal pia iliripoti kuwa IRGC imekuwa ikishauriana na makundi washirika wa Iran nchini Iraq, Yemen na Lebanon kuhusu uwezekano wa kuongeza mashambulizi katika kipindi hiki cha kupungua kwa mvutano, ikinukuu maafisa wanaofahamu tathmini za kijasusi za nchi za Kiarabu.

Kwa mujibu wa ripoti hiyo, makamanda pia wametumwa Yemen kuratibu na Wahouthi, na Iran imewapa taarifa pamoja na orodha ya maeneo ya kulenga, yakiwemo bandari na miundombinu ya nishati nchini Saudi Arabia.

Kwa mujibu wa maafisa wa Marekani, IRGC imeonya baadhi ya nchi za Ghuba kwamba iwapo Marekani itashambulia miundombinu kama hiyo nchini Iran, miundombinu yao ya nishati italengwa.

Vita vya Kiuchumi kati ya Iran na Marekani

A 3D image of a congestion of oil tankers and container ships in the Strait of Hormuz, causing disruption to maritime traffic.

Chanzo cha picha, Getty Images

Wakati Wall Street Journal ikilenga maandalizi ya Iran ya kuendeleza vita, New York Times iliandika katika ripoti nyingine kwamba vita vya Iran vimeingia katika hatua ambayo, zaidi yote, inafanana na "vita vya kiuchumi na mtihani wa utashi na uvumilivu wa pande zote mbili."

Gazeti hilo liliandika kuwa muda wa siku 60 uliowekwa baada ya makubaliano ya Juni, kwa ajili ya kufikia makubaliano mapana zaidi kuhusu kumaliza vita na mpango wa nyuklia wa Iran, kwa vitendo haupo tena.

Hivyo, mkakati wa Marekani umerudi tena kwenye vikwazo na kizuizi cha majini ili kuongeza shinikizo la kiuchumi dhidi ya Iran.

Mtazamo huu unafanana na sera ambazo Marekani imekuwa ikitumia mara kadhaa kuitenga Iran kiuchumi, ikiwemo wakati wa muhula wa kwanza wa Donald Trump. Hata hivyo, bado kuna kutokubaliana kuhusu iwapo shinikizo la kiuchumi pekee linaweza kuilazimisha Tehran kubadili msimamo wake.

Wiki hii, Waziri wa Hazina wa Marekani Scott Bessent alisema Washington inaandaa hatua mpya za kiuchumi dhidi ya Iran ambazo alisema zitakuwa kali zaidi kuliko zilizowahi kushuhudiwa.

Reuters iliripoti kuwa miongoni mwa hatua zinazozingatiwa ni kuongeza shinikizo kwa wanunuzi wa mafuta ya Iran pamoja na mitandao ya kifedha inayohusishwa na biashara ya nchi hiyo.

Lakini wakati huo huo, tofauti kubwa bado ipo: Iran inasema Marekani lazima kwanza itekeleze ahadi kama vile kuachilia mali za Tehran zilizozuiliwa, wakati utawala wa Trump unataka Iran iondoe vikwazo katika Mlango wa Hormuz kabla ya kuchukua hatua yoyote.

Kwa namna hii, pande zote mbili zinaonekana kucheza kamari huku wakivuta vuta muda, kila upande ukitumaini kwamba muda utamlazimisha mwenzake kufanya makubaliano zaidi. Hali hiyo imepelekea mkwamo katika mgogoro huo.

Mtihani wa uwezo wa Marekani kuvumilia vita

Lakini je, Marekani inaweza kuendelea na hali hii kwa muda gani?

Hilo ndilo swali lililoibuliwa Jumapili katika mahojiano ya kituo cha ABC na Admiral Mike Mullen, aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Wakuu wa Majeshi ya Marekani.

Katika kipindi cha "This Week" cha ABC, Mullen alizungumzia matumizi ya muda mrefu ya meli ya kivita Abraham Lincoln.

Alisema meli hiyo, yenye takribani wanamaji na wanajeshi 5,000, ilikaa baharini kwa siku 268 na haikuweza kusimama bandarini kwa zaidi ya siku 200 mfululizo.

Meli hiyo ilishiriki katika operesheni za kijeshi za Marekani katika vita vya Iran pamoja na kizuizi cha majini kinachohusiana na Mlango wa Hormuz.

Kwa mujibu wa Mullen, katika operesheni za kawaida, meli za Marekani zinaweza kuingia katika bandari za eneo hilo ili wanajeshi wapumzike, kufanya matengenezo na kupata mahitaji muhimu. Lakini vituo na maeneo ya Marekani nchini Bahrain, Kuwait na Umoja wa Falme za Kiarabu, ambavyo kwa kawaida hutumiwa kusaidia na kupumzisha wanajeshi, vimeshambuliwa na Iran wakati wa vita na haviwezi kutumika kama hapo awali.

Mullen alisema hata Diego Garcia, ambayo Marekani ilikuwa imeanza kuitumia kama kituo salama zaidi, imelengwa na Iran.

Kutokana na hali hiyo, imekuwa vigumu kupata maeneo salama ya kutia nanga meli, na vikosi vinalazimika kubaki baharini kwa muda mrefu zaidi.

Mullen pia alieleza kuhusu idadi ndogo ya meli za kubeba ndege za kivita zinazomilikiwa na Marekani. Jeshi la Wanamaji la Marekani lina meli 11 za aina hiyo, na Mullen alisema anaamini Marekani itahitaji zaidi iwapo Washington itaendelea kuzipeleka kwa kiwango kikubwa na kwa muda mrefu namna hii.

Alisema hali inayoendelea sasa inamaanisha "kujitolea" kwa baadhi ya uwezo wa kijeshi wa siku zijazo ili kukidhi mahitaji ya vita vya sasa.

Maoni ya umma yanataka nini kutoka kwa Trump?

Kadri vita vinavyoendelea na gharama zake za kiuchumi kuongezeka, kuna dalili kwamba uungwaji mkono wa vita hivyo unapungua, hata miongoni mwa wafuasi wa kisiasa wa Donald Trump.

Mwezi Mei, nusu ya wapiga kura wanaojitambulisha kama wafuasi wa MAGA waliamini kuwa vita dhidi ya Iran vilistahili gharama zake za kiuchumi, kwa mujibu wa kura ya maoni ya Politico iliyofanywa na taasisi huru ya Public First.

Sasa idadi hiyo imeshuka hadi zaidi ya theluthi moja tu, ikiwa ni imepungua kwa asilimia 13 ndani ya miezi miwili.

Aidha, asilimia 37 ya wafuasi wa MAGA wa Trump wanasema Marekani inapaswa kuendelea kushiriki katika vita hivyo iwapo tu havitasababisha gharama zaidi, ikilinganishwa na asilimia 29 mwezi Mei.

Karibu mmoja kati ya kila wapiga kura watano wa MAGA pia anasema Marekani inapaswa kumaliza vita na Iran, bila kujali gharama.

Takwimu hizi zinaonyesha kwamba upinzani dhidi ya kuendelea kwa vita, ambao awali ulikuwepo miongoni mwa sehemu kubwa ya maoni ya umma nchini Marekani, sasa umeenea hadi sehemu ya msingi wa kisiasa unaomuunga mkono Trump kwa karibu zaidi.

Katika mazingira hayo, Mbunge wa Republican na aliyewahi kuwa afisa wa Jeshi la Anga la Marekani, Don Bacon, alisema katika kipindi cha "Face the Nation" cha CBS kwamba Donald Trump ameunda "matarajio yasiyo ya kweli" kwa kurudia kusema kuwa makubaliano na Iran yako karibu kufikiwa.

Bacon alisema mwanzoni mwa vita kulikuwa na mtazamo kwamba mzozo huo ungeweza kumalizika ndani ya mwezi mmoja au miwili, lakini sasa ni lazima umma uelezwe wazi kwamba makabiliano na Iran huenda yakawa marefu zaidi kuliko ilivyotarajiwa awali.

Pia aliunga mkono kuendelea kwa shinikizo la kiuchumi na kizuizi cha majini, akisema Tehran ilitafsiri hamu ya Trump ya kufikia makubaliano haraka kama ishara ya udhaifu.

Bacon alimshauri Rais wa Marekani kuzungumzia kidogo uwezekano wa makubaliano na badala yake kuruhusu shinikizo la kiuchumi dhidi ya Iran kuendelea kuleta athari zake.

Hata hivyo, alionya pia kuhusu gharama za kuendelea kwa vita kwa Marekani yenyewe, ikiwa ni pamoja na kupungua kwa akiba ya baadhi ya silaha, zikiwemo makombora ya Patriot na cruise missiles.

Kauli za mbunge huyo wa Republican, pamoja na kura ya maoni ya Politico, zinaonyesha aina mbili za shinikizo zinazoukabili kwa wakati mmoja utawala wa Trump: kwa upande mmoja, baadhi ya wafuasi wa Trump wanamtaka aendelee na shinikizo la kijeshi na kiuchumi dhidi ya Iran; kwa upande mwingine, baadhi ya watu katika ngome yake ya kisiasa wanataka vita hivyo vikome na gharama zake zikomeshwe.