Iran yakabiliwa na kile Waziri wa Hazina wa Marekani, Scott Bessent, alichokiita "shambulio kubwa zaidi la kifedha kuwahi kutekelezwa", baada ya Marekani kutangaza mfululizo wa vikwazo dhidi ya Iran na kutishia nchi zinazoiunga mkono.
Bessent alieleza hatua hiyo kama "siku kubwa ya kiuchumi" kwa Iran, akisema Marekani itasitisha mahusiano yote ya kiuchumi na nchi hiyo. Aliongeza kuwa taifa lolote litakaloshirikiana kifedha na Iran pia litatengwa.
Hata hivyo, tishio hilo jipya dhidi ya serikali ya Iran linakuja baada ya Ikulu ya Marekani kubadili msimamo mara kadhaa na kuongeza muda wa makataa katika juhudi za kumaliza mzozo huo.
Kwa upande wake, Waziri wa Uchumi wa Iran, Ali Madanizadeh, alisema Tehran ina mpango wa miaka miwili wa kukabiliana na vikwazo hivyo, akidai mpango huo utasababisha Washington kushindwa tena.
Vita hivyo vimesababisha kupanda kwa bei ya mafuta duniani. Kufuatia tishio la hivi karibuni la Marekani, Iran imeonya kuwa inaweza kusitisha usafirishaji wote wa mafuta kutoka eneo hilo iwapo vita vitaendelea.
Serikali ya Iran pia imetoa onyo jipya kwa meli zinazopita katika eneo hilo, ikizitaka kutopita katika Mlango wa Hormuz bila ruhusa yake, kwa mujibu wa Reuters.
Kwa kawaida, takribani moja ya tano ya mafuta na gesi duniani hupitia Mlango wa Hormuz, njia nyembamba ya bahari iliyoko kusini mwa Iran. Hata hivyo, tangu kuanza kwa mzozo mwishoni mwa Februari, Iran imezuia kwa kiasi kikubwa usafirishaji kupitia njia hiyo, hatua iliyochangia kupanda kwa bei ya mafuta duniani.
Katika mkutano na waandishi wa habari Jumatatu, Bessent alieleza kile Marekani imekiita "Operesheni ya kuwatenga kiuchumi", akisema Washington inaanzisha "shambulio la kiuchumi dhidi ya miunganisho ya kifedha ya Iran kote duniani".
Bessent alisema Iran sasa inakabiliwa na chaguo mbili zilizo wazi: "kutengwa kabisa na dunia" au kurejea katika hali ya kawaida na kupata fursa ya kujiunga tena na uchumi wa dunia.
Waziri huyo wa Hazina alisema Marekani "haitawali tena tishio la Iran, bali inalimaliza".
Bessent alisema Wizara ya Hazina ya Marekani imebaini mitandao, wawezeshaji na njia za kifedha zinazotumiwa na Iran kukwepa vikwazo na kuendelea kufanya biashara ya mafuta.
Wizara hiyo imesema imechukua hatua dhidi ya sekta tano, ambazo ni mali za kidijitali, teknolojia, dhahabu, usafiri wa anga na usafirishaji wa majini.
Aidha, Hazina ya Marekani imetangaza vikwazo dhidi ya karibu taasisi, watu binafsi na meli 60 zinazohusishwa na Iran.