Moja kwa moja, Mafuriko Nepal na Tibet yaua zaidi ya watu 160, mamia ya watalii hawajulikani walipo

Mamia ya watu hawajulikani walipo baada ya mafuriko Nepal, baadhi ni wakimbizi

Muhtasari

Moja kwa moja

Na Beldeen Waliaula

  1. Marekani na UN zatoa msaada kwa waathiriwa wa mafuriko Nepal

    .

    Chanzo cha picha, EPA

    Marekani imeahidi kutoa msaada wa dola 500,000 ambazo zitatumika kugharamikia makazi ya muda, maji, huduma za usafi na misaada mingine kwa jamii zilizoathiriwa na mafuriko.

    “Marekani inatuma salamu zake za rambirambi kwa familia na jamaa wa waliofariki katika mafuriko makubwa ya ghafla yaliyoikumba wilaya ya Rasuwa nchini Nepal,” Idara ya Mambo ya Kigeni ya Marekani ilisema katika taarifa.

    Takriban raia 54 wa Marekani, wengi wao wakiwa watalii, wameripotiwa kuwa miongoni mwa mamia ya watu waliopotea kufuatia mafuriko na maporomoko ya ardhi.

    Hayo yakijiri, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, amesema “amehuzunishwa na mafuriko hayo makubwa” ambayo yamesababisha vifo vya watu wengi, huku wengine wakiwa hawajulikani walipo nchini Nepal na China.

    “Nasimama pamoja na wote walioathiriwa,” amesema kiongozi huyo.

    Ameongezea kuwa timu za Umoja wa Mataifa na washirika wake zinaandaa kusafirisha vifaa pamoja na kuwapeleka wahudumu wa dharura nchini Nepal ili kuisadia kukabiliana na janga hilo.

    Soma pia:

  2. Tazama namna vijiji vilisombwa na mafuriko Nepal

    Maelezo ya video, Picha za angani zaonyesha mafuriko makubwa katika mpaka wa Nepal na Tibet

    Waokoaji wanakabiliwa na changamoto kufika katika maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko makubwa ya ghafla na maporomoko ya udongo nchini Nepal, ambayo yamesababisha vifo vya zaidi ya watu 160.

    Mamia ya watalii hawajulikani walipo, wakiwemo zaidi ya 100 kutoka India, 54 kutoka Marekani, 34 kutoka Australia na 33 kutoka Uingereza.

    Maafisa pia wanasema zaidi ya watu 100 kutoka Nepal wenyewe hawajulikani walipo.

    Eneo hilo ni maarufu kwa watalii wanaofanya matembezi milimani pamoja na mahujaji.

    Wakati shughuli za uokoaji zikiendelea, wataalamu wanaonya kuwa vifusi vilivyoziba mto karibu na eneo la maafa vinaweza kusababisha mafuriko mengine.

    Mamlaka zinaendelea na juhudi za kuwasaka na kuwaokoa watu waliokwama katika maeneo yaliyoathiriwa.

  3. Iran yaishtumu Marekani kwa kujaribu kuzuia mazungumzo yao na Oman

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Jeshi la Iran IRGC, limeishtumu Marekani kwa kile wamekitaja ‘kujaribu kuzuia’ makubaliano kati ya Iran na Oman, kuhusu usimamizi wa Mlango Bahari wa Hormuz.

    Jeshi hilo limesema wamefikia makubaliano na Oman, ya kugawana mapato watakayokusanya katika usimamizi wao wa Pamoja wa Mlango wa Hormuz,ila Marekani inajaribu kuzuia kukamilika kwa makubaliano hayo.

    Tehran na Muscat zimejadili kuanzishwa kwa njia nyingingine ya bahari na mfumo utakaoendesha safari za meli katika Mlango wa Hormuz.

    Aidha, Tehran imeonya kuwa njia hiyo ya bahari haitafunguliwa tena hadi Marekani isitishe vita.

    Mazungumzo kati ya Iran na Oman, yanajiri baada ya Washington kutangaza vikwazo vipya vinavyolenga kuilemaza Iran kiuchumi.

    Soma pia:

  4. Mafuriko Nepal na Tibet yaua zaidi ya 160, mamia ya watalii hawajulikani walipo

    D

    Chanzo cha picha, Reuters

    Zaidi ya watu 160 wamefariki nchini Nepal, huku mamia ya watalii wakiwa hawajulikani walipo baada ya mafuriko makubwa ya ghafla na maporomoko ya udongo katika eneo la mpaka kati ya Nepal na Tibet.

    Nchini China, idadi ya watu ambao hawajulikani walipo baada ya maporomoko ya udongo katika kaunti ya Gyirong, Tibet, imefikia 558, kwa mujibu wa shirika la utangazaji la serikali CCTV.

    Kati yao, 260 ni raia wa kigeni. Idadi ya waliofariki imeendelea kuwa watatu.

    Mpaka wa Gyirong ni njia kuu inayotumiwa na watalii na magari kusafiri kati ya China na Nepal.

    Nepal awali ilisema watu 579 hawajulikani walipo, wakiwemo raia 466 wa kigeni. Haijafahamika mara moja iwapo baadhi ya watu hao wamehesabiwa mara mbili katika takwimu za nchi hizo mbili.

    Jeshi la Nepal limetuma wanajeshi 2,000 kushiriki katika shughuli za utafutaji na uokoaji kwa njia ya ardhini na angani katika maeneo yaliyoathiriwa na mafuriko.

    Msemaji wa jeshi, Brigedia Jenerali Rajaram Basnet, ameiambia BBC kuwa wanajeshi hao wamejikita katika maeneo yaliyoathirika zaidi, yakiwemo wilaya za Rasuwa na Nuwakot.

    Jeshi hadi sasa limefanikiwa kuwaokoa watu 97 waliokuwa wamekwama kwenye mafuriko. Watatu kati yao walikuwa wafanyakazi waliokwama katika handaki la mradi wa kuzalisha umeme wa maji wa Trishuli A.

    Polisi na kikosi cha polisi wenye silaha cha Nepal pia vimepeleka maafisa katika maeneo yaliyoathiriwa kusaidia shughuli za utafutaji.

    Awali mamlaka zilidhani kuwa huenda tetemeko la ardhi lilitangulia mafuriko hayo. Hata hivyo, Utafiti wa Jiolojia wa Marekani, USGS, sasa umesema nishati iliyosababisha mtikisiko huo ilitokana na maporomoko ya udongo, badala ya tetemeko la ardhi.

  5. Waziri Mkuu wa Qatar kuzuru Tehran

    .

    Chanzo cha picha, Getty Images

    Waziri Mkuu wa Qatar anatarajiwa kuzuru Tehran hii leo, katika juhudi za kuanzisha tena mazungumzo ya kidiplomasia, baada ya makubaliano ya kusitisha vita kati ya Iran na Marekani kuvunjika.

    Washington tayari imetangaza kuiwekea Iran vikwazo vya kiuchumi pamoja na washirika wake wa karibu.

    Qatar, ambayo ni jirani wa Iran katika eneo la Ghuba na pia mshirika wa Marekani, imekuwa mpatanishi wa siri kati ya pande hizo mbili zinazozozana, na ilichangia pakubwa katika kufanikisha makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyoafikiwa mwezi Juni.

    Ziara ya Waziri Mkuu wa Qatar, Mohammed bin Abdulrahman bin Jassim bin Jaber Al Thani, inafanyika wakati vita kati ya Iran na Marekani vinaingia mwezi wake wa sita huku kukiwa hakuna dalili ya mafanikio yoyote ya kidiplomasia.

    Marekani na Iran bado zinatofautiana kuhusu Mlango Bahari wa Hormuz ambayo ni njia muhimu ya usafirishaji mafuta duniani.

    Soma pia:

  6. Hujambo na karibu katika matangazo yetu ya moja kwa moja Alhamisi ya leo